Matokeo bora ya zoezi hili la Uchaguzi Mkuu utakaofanyika siku ya Jumatano Oktoba 29, 2025 yanategemea zaidi umakini na uelewa wenu katika mafunzo haya mnayopatiwa leo, hivyo ninawasihi kufanya kazi kwa uadilifu na mkitambua kuwa nyinyi mliopo hapa mmeteuliwa kwa mujibu wa sheria, na tangu tarehe ya uteuzi wenu mnao wajibu wa Kikatiba na mmeaminiwa na Tume ili kutekeleza majukumu ya uchaguzi kwa kuwaongoza Wananchi waweze kuchagua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mbunge na Madiwani kwa niaba ya Tume katika vituo vya kupigia kura mtakavyopangwa.
Hayo yamesemwa leo Oktoba 25, 2025 na Ndg. Emmanuel Richard Mpongo Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Monduli katika Ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii (CDTI) wakati akifungua mafunzo kwa Makarani waongozaji wapiga kura Jimboni humo; watakaofanya shughuli za Uchaguzi katika jumla ya vituo 400 vilivyopo kwenye kata 20 za Halmashauri ya Wilaya ya Monduli huku akiwasisitiza kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo katika Uchaguzi huo.
Aidha, Ndg. Mpongo amewaeleza Makarani hao kuwa wameapa viapo vya Uaminifu na Uadilifu na hivyo wanapaswa kuzingatia maelekezo na kufanya kazi kwa weledi ikiwa ni pamoja na kuwahi katika vituo vya kupigia kura saa 12:00 asubuhi na kuzingatia muda maalumu wa kufunga vituo hivyo kama ilivyoelekezwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi.
Naye Bi. Jakline Mbwango kwa niaba ya Mkuu wa TAKUKURU Wilaya ya Monduli, amewataka Makarani hao kutokupokea wala kutoa zawadi au ahadi yoyote wakati wa uchaguzi, huku akiwasisitiza Makarani hao kufanya kazi zao za uongozaji na usimamizi katika uchaguzi Mkuu kulingana na maelekezo ya Tume.
Teddy Sante, mmoja wa Makarani waongozaji wa Jimbo la Monduli, amesema, mafunzo aliyoyapata anaamini yamemsaidia kuongeza uelewa kuhusu namna bora ya kuwaongoza wapigakura na anaahidi kuwa atatekeleza majukumu yake kwa weledi na kwa mujibu wa maelekezo aliyopatiwa.
Monduli District Council
Sanduku la Posta: P.O BOX 1 Monduli
Namba ya simu: +255 - 27- 2538006
simu ya mkononi:
Barua Pepe: ded@mondulidc.go.tz
Hatimiliki @2017 Halmashauri ya Wilaya ya Monduli