Vijana mnaohitimu mafunzo yenu leo, ni Imani yangu kuwa mmejifunza Uzalendo, Utii, Ukakamavu na mafunzo ya kijeshi kwa dhana ya Ulinzi na Usalama wa nchi yetu. Hivyo ni vema mkayatumie vizuri ili kutimiza lengo la Taifa la kuwaandaa kuwa Jeshi la akiba na kamwe msilaghaike kujiunga na vikundi vya uhalifu kwa kuwa mtakuwa wasaliti wa Taifa ambalo limetumia gharama kubwa kuwaandaa.
Hayo yamesemwa leo Septemba 24, 2025 na Mhe. Gloriana Kimath Mkuu wa Wilaya ya Monduli wakati akifunga rasmi mafunzo ya awali ya JKT Kundi la lazima la mujibu wa Sheria la Vijana wa Oparesheni Nishati Safi, yaliyofanyika katika Viwanja vya 839, JKT Makuyuni.

Naye Kamanda wa Kikosi cha 839 JKT Makuyuni Luteni Kanali Andrew Lwanda amesema kuwa vijana hao wameandaliwa vema na wamekuwa wasikivu na watii katika kupokea maelekezo waliyopewa. Huku akieleza kuwa lengo la mafunzo waliyoipata ni kuwawezesha kuwa wazalendo, shughuli za ujasiriamali na uzalishaji Mali sambamba na Ulinzi wa Taifa la Tanzania.

Akisoma Risala kwa niaba ya wahitimu wenzake, Kuluti Fatuma Abas Magati; ameeleza faida mbalimbali walizopata kutokana na mafunzo hayo lakini pia changamoto walizokabiliana nazo kuwa ni pamoja na uvamizi wa Wanyama pori, changamoto ya umeme na maji pamoja nayo changamoto ya miundombinu ya barabara kuu ya kuingia kikosini.

Kupitia Risala hiyo Kuluti Fatuma Abas ameomba kuwa, suala la uvamizi wa wanyamapori Serikali isaidie kuchimba bwawa kubwa la Maji mbali na Kikosi ili Wanyama wapate maji nakuacha kuingia kikosini, kuweka sawa miundombinu ya barabara huku akitoa Rai kwa Serikali kuyafanya mafunzo hayo endelevu na kwamba wao wako tayari kutumika kwa kadri Taifa litakavyoona inafaa.

Mhe. Gloriana ameagiza Meneja RUWASA,TARURA na Idara ya Wanyamapori kuhakikisha wanazifanyia kazi changamoto zote zilizoelezwa na kuahidi kufuatilia utekelezaji wake.
Kwa upande wake, Mwalu Gumada Ghushaha mhitimu na mzawadiwa wa zawadi za jumla katika masomo ya darasani, zoezi la kulenga shabaha, usafi, medan na kwata ; ameeleza furaha yake kwa kuhitimu, nakueleza kuwa mazuri yote waliyojifunza watayafanyia kazi na kuahidi kuwa wazalendo popote watakapo kwenda.

Monduli District Council
Sanduku la Posta: P.O BOX 1 Monduli
Namba ya simu: +255 - 27- 2538006
simu ya mkononi:
Barua Pepe: ded@mondulidc.go.tz
Hatimiliki @2017 Halmashauri ya Wilaya ya Monduli