Kuna faida nyingi anazopata Mwananchi aliyejiunga na mfuko wa BIMA ya Afya kwa wote, ikiwemo kupata huduma mahali popote nchini kuanzia ngazi ya zahanati, vituo vya Afya, hospitali ya Wilaya na hospitali za rufaa kwa kujiunga na kitita cha shilingi 150,000/= tu kwa kaya yenye jumla ya watu sita (6).
Hayo yamesemwa leo Januari 19, 2026 katika Ukumbi mkubwa wa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli na Mhe. Gloriana Julius Kimath Mkuu wa Wilaya hiyo, katika kikao kilichojumuisha viongozi, na makundi mbalimbali wakiwemo: wawakilishi wa wazee, watu wenye ulemavu, viongozi wa dini, viongozi wa kimila (malaigwanani), wafanya biashara, CMT na CHMT, Mabodaboda, Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya, Taasisi na Katibu wa Chama cha Mapinduzi Wilaya.
Akitoa wa wasilisho la BIMA ya Afya kwa wote Bi.Gloria Mziray Afisa Uanachama BIMA ya Afya Mkoa amesema kuwa, kila Mwananchi ana haki ya kupata huduma bora na BIMA ya Afya kwa wote ndilo suluhisho la kupata matibabu bora kwa wote.
Aidha,ameeleza kuwa kupitia kifurushi cha faraja kila mwananchi anayofursa ya kujiunga na kupata huduma sawa kwa kuchangia shilingi laki moja na nusu (150,000l=) kwa Kaya ya watu 6 yaani Mkuu wa Kaya ,Mwenza na wategemezi wanne. Ambapo kadi za NIDA zitatumika kadhalika na asiye na NIDA atapewa namba maalum ya kwenda kutibiwa wakiwemo watoto.
Kwa upande wake Ndg.Miraji Kisire ambaye pia ni Afisa UANACHAMA Mkoa Arusha ameeleza kuwa kwa kitita cha shilingi 150,000/= wananchi wanasajiliwa kupitia ngazi za chini kwa mawakala wakusajili laini za simu au Taasisi za kifedha ambao pia wanapewa Elimu ya namna ya kusaliji Wananchi katika BIMA ya Afya kwa wote.Aidha,ameeleza huduma anazopata Mwananchi kupitia kitita cha sh.Laki 150,000 kuwa ni huduma za kujiandikisha kumuona Daktari hadi Daktari Bingwa, kupata vipimo vya maabara, X-ray, ultrasound, damu, sukuri na vifaa tiba zaidi ya 207, upasuaji mkubwa na mdogo, na gharama za kulazwa.
Kwa upande wake Dkt. George Kasibante ambaye ni Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli amefafanya kuwa mapungufu yaliyokuwepo kwenye BIMA ya Afya iliyoboreshwa kwa upande wa huduma ambazo hazikuwepo, sasa zinapatikana kwenye kitita cha BIMA ya Afya kwa wote. Baada ya kijisajili na kulipia ndani ya siku 30, Mwananchi ataweza kupata huduma za Afya bila changamoto.
Dkt. Kasibante, Ameongeza kusema kuwa ifikapo Juni au Disemba, 2026 Halmashauri hiyo itakuwa imeongeza vituo vingine vya Afya vitatu kikiwemo kituo cha Afya Sepeko, Engaruka na Lolkisale ili kusogeza huduma kwa wananchi kutokana na umbali wa vijiji katika maeneo hayo. Hivyo amewaomba Wananchi hasa waliohudhuria kikao hicho kwenda kuwa mabalozi Wazuri katika kuelimisha na kihamasisha Wananchi kujiunga na mfuko wa BIMA ya Afya wa Kitita cha shilingi 150,000/= kwa kaya ya watu sita.
Naye Bi. Happiness R. Laizer Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli amesema "Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliahidi kuwa ndani ya siku 100 za Uongozi wake ataajiri Watumishi wa Idara ya Afya na Elimu; hivyo ninapenda kuwataarifu kuwa katika mwezi huu wa kwanza Mhe. Rais ametimiza ahadi yake kwa kutupatia Watumishi wa ajira mpya 79 katika Idara ya Afya na ninaamini watakwenda kupunguza changamoto ya upungufu wa Watumishi katika vituo vyenye Watumishi wachache ili kuendelea kuboresha huduma za afya" amesema Bi. Happiness Laizer
Sambamba na mapokezi ya ajira mpya 79 za kada ya Afya, Mhe. Kisioki Lengoije Moitiko Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo amesema kuwa, anamshukuru Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ajira mpya hizo alizotoa kwa Halmashauri ya Monduli, kwani tiyari Kuna zahanati nne za Engorika, Ranch na Nengipima ambazo ziko hatua za ukamilishwaji na zinatarajiwa kuanza hivyo kwa uwepo wa wataalamu wa kutosha, tunatarajia Wananchi wengi watapata huduma bora za BIMA ya Afya.
Yohana Minadi Sikane, kwa niaba ya madereva Bodaboda walioshiriki kikao hicho, Amemshukuru sana Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuwakumbuka Wananchi wa Monduli kwa suala la BIMA la ya Afya kwa wote na ameahidi kuwaelimisha na kuwahimiza na Bodaboda wenzake kujiunga na mfuko huu wa BIMA ya Afya kwa wote.
Monduli District Council
Sanduku la Posta: P.O BOX 1 Monduli
Namba ya simu: +255 - 27- 2538006
simu ya mkononi:
Barua Pepe: ded@mondulidc.go.tz
Hatimiliki @2017 Halmashauri ya Wilaya ya Monduli